Powered By Blogger

Saturday, April 28, 2012

KWANINI
HABA NA HABA BBC Swahili NA SI TBC Taifa?

Kipindi maridhawa kilichoanzishwa tarehe 24 machi na Idhaa ya Kiswahili BBC cha Haba Na Haba ( Little by Little) hakina budi kunizushia mjadala binafsi ya kuwa kwa nini Shirika la Habari la Uingereza ndio limeweza kuchukua fursa na wasaa huo badala ya watanzania kuweza kutumia vyombo vyao vya habari kama TBC kuwa ndio daraja madhubuti la kupitishia malalamiko, vilio, mikasa, raha, furaha na shangwe zao kwa viongozi?

TBC na vyombo vingine vya habari nchini hhaviana uwezo wa kuwakutanisha watanzania na viongozi mpaka BBC watufanyie hatuwezi kuwa makini namna hiyo kwa mintaarafu ya kutafuta na kujua mstakabali wa taifa la tanzania kama tunashindwa kufanya jambo kama hili. hii ni dalili tosha kuwa ama kweli tanzania haina waandishi wabunifu kama ilivyo katika vyombo vingine vya habari kimataifa. hoja hii inaweza kushaijishwa na mlolongo wa vipindi vingi vya muziki si katika redio wala runinga ambavyo dhima yake kubwa ni kuburudisha tu na kumfanya mwananchi wa kawaida ashindwe kukaa na kutathmini namna atakavyoweza kupambana na mabadiliko haya ya kidunia, kukua kwa kasi kwa sayansi na teknolojia, mabadiliko ya tabia nchi, ongezeko la watu duniani, uharibifu wa mazingira na majanga mbalimbali. Si redio wala Runinga ambayo imethubutu kuandaa vipindi aushi kwa kuielimisha jamii namna ya kuja kupambana na changamoto za Muungano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, la hasha...

Vyombo vya habari huchukuliwa kama ndio nguzo ya nne katika mfumo wa uongozi nchini ukiongozwa na serikali kuu, bunge na mahakama japo Msomi mwenye kuhusudu siasa za wastani, mwanasheria na mwandishi Profesa Issa Shivji hasiti kuviweka angani vyomo hivyo kuwa ni nguzo ya kwanza kwa mintaarafu ya maslahi ya jamii. Kipindi cha Haba na Haba huangazia mashakili mengi yanayowasibu watanzania na kujaribu kuyafikisha mateso hayo kwa wawakilishi wao kuanzia ngazi ya kijiji hadi ya taifa. Tangu kianzishwe kimeanika matatizo mbambali nchini tena yaliyopo mbali na jiji la Dar-es-Salaam kama tatizo la maji, vitanda hospitalini, vifaa, madarasa pamoja na walimu katika shule za msingi nchini pamoja na tatizo miundombinu. Haya ni masahibu makubwa mno ambayo si kweli kuwa kama taifa la Tanzania lingekuwa na viongozi wote wazalendo kama walivyo baadhi suluba hizi zisingepungua kwa asilimia zaiidi ya sabini. Ukichimba sana utagundua kuwa haya masuala yote yanatatulika ikiwa kutakuwa na UTAWALA BORA ambao ndio dhamira kuu ya kipindi cha haba na haba. Neno utawala au uongozi bora ni kama vile halipo si tu katika kamusi ya TUKI bali hata katika vitabu tukufu vya Injili, Qur'an na Biblia kwa viongozi wa kiafrika...

Haba na Haba ni moja ya kipindi kinchoamsha na kuwaletea changamoto waandishi wa kitanzania kuwa hawana budi kukaa chini na kuanzisha vipindi vyenye kuelimisha jamii ili kuweza kufikia malengo ya Milenia kama si kupiga hatua na kufikia nchi kama Indonesia, Singapore, Afrika Kusini na India kimaendeleo. Vyombo vya habari ni moja taswira inayosadifu uwezo wa fikra wa jamii fulani. Waandishi wekeni Utaifa mbele kwanza...

Mtangazaji wa kipindi hiko mujarab Hassan Mhelela amesema ana furaha kubwa kuwa sehemu ya kipindi hiko ambacho ni jukwaa la heshima la kuwawajihisha watanzania na viongozi.

Haba na Haba hutangazwa na BBC Swahili saa 10.05 alasir kwa saa za Afrika Mashariki, jumamosi na jumapili saa 12 asubuhi.Unaweza kukisikiliza kupitia tovuti ya bbcswahili.com.


Sunday, April 15, 2012

MAREHEM KANUMBA NA FUNZO KWA VIJANA TANZANIA

Marehem Steven Charles Kanumba ( 1984-2012)
Tarehe 7 Aprili mwaka 2012, itakuwa siku ya kukumbukwa sana hasa kwa waigizaji wa filamu Tanzania almaaruf Bongo Movies baada ya kumpoteza kipenzi na msanii mwenzao Steven Charles Kanumba.
Marehem Steve aliyependa kujiita The Great lenye maana sawa na Wonderful au maridhawa kwa lugha ya kiswahili chepesi kitu kizuri, shani, kupendeza na thamani kifupi Shujaa.
Jina hilo la utani halikuacha kuwa sanjari na mjiitaji husika, kwani hakuwa maridhawa tu bali alipanda maghorofa kadhaa ya juu.
Tathmini ya namna ya uigizaji wake, vituko, mizaha yake iliyonakshiwa na haiba jamali aliyoshaijishwa na Malik.
Maandishi hayatoshi kumuelezea kama mwigizaji, matayarishaji na mwanamuziki alikuwa na talanta ya pekee kwa watanzania pamoja na waafrika kiujumla.
Filamu ni moja ya sanaa ya kipekee duniani ambayo ndani yake utakuta kila makabila kadhaa ya sanaa kama muziki, fasihi, ususi, ufumaji, uchoraji n.k.
Sinema alizowahi kufanya marehem zinakadiriwa kufika mia moja (100) zilikuwa na zitakuwa zikimuanika na kumuonyesha kuwa alichukulia sanaa ile kama uwanja ambao angeweza kuutumia zaidi kuelimisha na kuitangaza jamii yake hata kimataifa.
Katika filamu zake aliweza kusadifu mambo mengi yanayowazuzua waafrika wengi hasa sula la mapenzi, ugumu wa maisha pamoja na upotoshwaji na usahaulifuwaji wa mila na desturi za kitanzania.
haitoshi kuwaanika wanawake wakiwa nusu uchi waliojawa na ubinafsi sura na taswira iliyopo kwa wasichana wengi wa kitanzania.
Hakuwa tu msanii yule aliyetakwa na jamii bali yeye ndo alijikaramia kwa jamii yake hasa. Kauli yake ya kuwa aliichukulia tasnia hiyo kama baba na mama yake ilijidhihirisha katika uwezo wake wa kubuni, kuigiza na hata namna ya kufikisha ujumbe katika jamii yake.
Kifo cha nyota huyu ni pigo kimeacha pengo kubwa katika sanaa ya tanzania kijumla kwani hakujifungisha ndoa tu na filamu bali na muziki vilevile.
Kanumba anatoa mafunzo kama kijana aliyekataa kusema hapana na aliyeshinda kulala kwa kuridhika na mafanikio aliyowahim kuyapata. Kitendo cha kushirikiana na waigizaji kutoka nigeria ni ishara tosha kuwa shujaa huyu alijiona hajafanya lolote kwa jamii yake hivyo daima alijiona yu njiani.
Alikuwa mchapakazi hasa kwani si ajabu kuona ushiriki wake katika kipengele zaidi ya kimoja katika sinema alizowahi kufanya. Suala la kuwa hata balozi wa star times pia ni elimu kwani tanzania ina wasanii wangapi lakini kwanini kampuni ile ilimuomba kuwa taswira ya matangazo ya bidhaa zao ambayo bado aliing'arisha.
yumkini hata kama haitoshi kuwa mwakilishi wa shirika la misaada ya Uingereza la Oxfam nichini Tanzania bado inashawishi kuwa ama hakuna anayepinga kuwa taifa limempoteza kijana aliyejua wapi anatoka na wapi anaelekea.
Aliyewahi kuwa bondia maarufu duniani Muhammad Ali aliwahi kusema kuwa ni vigumu kuwa mnyenyekevu kwa watu hasa kama utakuwa shujaa kama yeye. Muhammad ni mtu mpole sana pamoja na historia ya ajabu aliyoweka katika ulingo duniani lakini bado aliithamini na kuisikiliza jamii yake kinyume na baadhi ya watu wakishapanda vichuguu kidogo basi hujawa na viburi, dharau, majivuno, tambo na tadi na kejeli kwa walimwengu wenzao.
Marehemu Kanumba anaingia katika tabaka la watu ambao wala hawakuwahi kuingiwa kichwani na umaarufu kwani alikuwa mpole, msikivu, mwenye aibu ya wastani, hekima na busara sifa ambazo waeza kuziona kupitia hata alipokuwa akifanyiwa mahojiano katika vituo mbalimbali vya runinga hapa nchini.
chanzo cha kifo chake kimezua mjadala na sura picha mbaya miongoni mwa watanzania japo kuna hatua ambayo wengi tunaisahau kuwa hakuna hata mtu mmoja katika dunia anayejua namna atakavyokufa ama kurejea kwa Bwana Muumba. laiti tungekuwa tunajua namna tutakavyofariki hakika hakuna kiumbe yoyote angethubutu kujishughulisha na jambo lolote la kimaendeleo bali kuwazia namna atakavyoikabili siku hiyo.
Si lazima kuangalia ubaya wa mtu au wa kitu, marehemu Kanumba katuachia changamoto nyingi sana sisi vijana wa kitanzania, tujaribu kutathmini uzuri na mchango aliojaaliwa kuufanya kwa taifa la tanzania ili mimi, yule, wewe, wao hatuna budi kifikiria namna na sisi tutakavyoweza kukumbukwa kama vijana tuliojaribu kuifanya jamii yetu iache kuishi inavyoishi na kuishi namna inavyopaswa kuishi.

BASATA haina budi kumuenzi Marehem Kanumba hata kwa kumfungulia wakfu ( Foundation ) utakaokumbuka yale yote aliyoyahimiza katika kuendeleza sanaa ya uigizaji Tanzania. Hata tovuti maalum itakayohifadhi falsafa zake dhiki ya kukwamua uwanja huo wa burudani nchini, tovuti hiyo iwe na picha, vidio zake na mahojiano yake kama urithi kwa kizazi kitakachokuja ili kumuenzi na kumkumbuka Baba huyu wa Filamu Tanzania.

"Watu wenye vipaji ndio hufanikiwa maishani lakini kati ya hao ni wale wachapakazi tu"- Quincy Jones Jr, mtayarishaji, mwelekezaji na mpangaji wa muziki nchini Marekani .

Friday, April 6, 2012

UJIO WA PROF. A. ABDALLA UDSM, TANZANIA

Ni mmoja ya mwanafasihi, mpenzi wa lugha adhwim na aula ya kiswahili niliyotokea kumhusudu katika ujana wangu hasa tangu niingiwe na mdudu wa kukipenda na kukienzi kiswahili.
Si mwingine bali ni yule mshairi, mhadhiri na mtangazaji Profesa Abdilatif Abdalla kutoka Mombasa, Kenya aliyewahi kufungwa jela kuanzia mwaka 1969-1972 katika gereza la Kibiti nchini Kenya baada ya serikali ya Jomo Kenyatta kumtia hatiani eti kisa aliandika ukweli kuhusu hofu na wahaka dhidi ya uongozi wake katika kabrasha la Kenya Twendapi.
Profesa Abdala atakuwepo nchini Tanzania akitokea nchini Ujerumani alikokua akifundisha lugha ya kiswahili katika Chuo Kikuu cha Leipzig katika mhadhara utakaofanyika katika Chuo Kikuu kikongwe cha Dar-Es-Salaam. Akiwa kama mmoja wa wahadhiri siku hiyo ya Ijumaa ya tarehe 13, Aprili mwaka huu katika ukumbi wa Nkrumah, Osagefyo, Profesa atachimba hasa na kutoa vumbi dhidi ya mchango kuntu unaotolewa na wasanii katika ukombozi wa bara la Afrika.
Profesa Abdilatif Abdalla 
Mhadhara huo utaanza rasmi saa 2 asb ila Gwiji mwenyewe atapamba na kuling'arisha jukwaa majira ya saa 3 unusu.

Wote mnakaribishwa.